Friday, June 10, 2016

KISUKARI CHA UKUBWANI KINAWEZA KUTIBIKA - KULA LISHE SAHIHI




Kisukari cha ukubwani ni nini?

Kisukari cha ukubwani ni hali inayojitokeza pale mwili wako unaposhindwa kuchakata sukari aina ya glucose na hivyo kuifanya ilundikane kwenye damu, badala ya kwenda katika seli za mwili ili itumike kuzalisha nishati ya kuendeshea shughuli za mwili. Mlundikano huu wa sukari kwenye damu una madhara mengi sana kiafya, kiasi kwamba hatua zisipochukuliwa kuondoa mlundikano huo kwenye damu, madhara hayo yanaweza kuishia kusababisha magonjwa hatari yanayoweza kupelekea kwenye ulemavu na kifo.

Magonjwa yenye uhusiano na mlundikano wa sukari kwenye damu ni yapi?

Baadhi ya magonjwa yenye uhusiano na mlundikano wa sukari kwenye damu ni shinikizo la juu la damu (hypertension), ugonjwa wa moyo, ugonjwa wa figo, ugonjwa wa ini, uharibifu wa mishipa ya damu na ile ya fahamu, uharibifu wa macho, uharibifu wa ubongo, na maambukizi ya mara kwa mara ya vimelea vibaya vya maradhi hasa tumboni na kwenye njia ya haja ndogo. Aidha ni rahisi kwa mtu anayekabiliwa na mlundikano wa sukari kwenye damu kushindwa kupona majeraha na hivyo kuwa katika hatari ya kupoteza viungo vya mwili, ikiwa ni pamoja na kupata upofu.

Sababu za kisukari cha ukubwani

Sababu za kisukari cha ukubwani ziko nyingi. Hapa tutazungumzia moja nayo ni kiungo kinachoitwa kongosho kushindwa kuzalisha homoni ya insulin ya kutosha. Insulin ndiyo homoni inayofanya kazi ya kubeba sukari na kuisafirisha kutoka kwenye damu na kuiingiza katika seli za mwili. Hii insulin inazalishwa na kundi la seli zinazopatikana kwenye kongosho zinazoitwa beta. Seli hizo zinaposhindwa kufanya kazi kwa sababu moja au nyingine kiasi cha isulin kinachozalishwa hupungua sana na hivyo kusababisha sukari ianze kulundikana kwenye damu.

Uharibifu wa kongosho.

Kumefanyika tafiti nyingi zilizolenga kubaini chanzo cha seli za beta kushindwa kazi. Baadhi ya hizi tafiti zimebaini kuwa maambukizi katika kongosho, hususan yanayotokana na virusi yanaweza yakaharibu seli hizi na hivyo zikaacha kufanya kazi. Hata hivyo tafiti nyingi zimebaini kuwa sababu kubwa ni uchovu. Tafiti hizi zimebaini kuwa kutokana na ulaji wa wanga uliopitiliza mipaka, hasa ule uliochakatwa (wali mweupe, sembe, chapati, mikate, chips, keki, sukari, soda, nakadhalika), seli hizi hupambana kuzalisha insulin ya kuondoa mzigo wa sukari unaoingia mwilini kila mara kupitia vyakula hivi, lakini hatimaye huzidiwa nguvu na kunyoosha mikono!

Kongosho linaweza kutibika!

Bahati nzuri tafiti zimebaini pia kuwa kisukari kinachokuja kutokana na mazingira haya kinaisha iwapo seli za beta zitapewa muda wa kutosha kupumzika. Imebainika kuwa seli hizi huanza tena kuzalisha insulin ya kutosha pale uchovu ziliokuwa nao unapomalizika. Ili kuzipumzisha seli zako za beta kuna haja ya kuondoa kabisa vyakula vinavyozalisha glucose kweye lishe yako. Miongoni mwa hivi ni hivyo tulivyotangulia kuvitaja katika paragraph iliyotangulia. Ili kupata nishati ya kutosha katika kipindi hiki utahitajika kuongeza kiasi cha mafuta bora ya kula kwenye kila mlo wako. Kumbuka mafuta bora zaidi ni yale ambayo ni koza (saturated fats) ikiwa ni pamoja na nazi, mafuta ya zaituni (olive oil), na siagi (butter). Mafuta ambayo siyo koza (polyunsaturated fats) kama yale ya alizeti yanaweza kufaa pia alimradi tu iwapo yataliwa katika hali ya ubichi. Hii ni kutokana na ukweli kwamba mafuta haya yanapopikia hubadilika na kutengeneza mafuta tenge (trans fats) ambayo tafiti zimebaini kuwa yanapoingia mwilini hulundikana kwenye mishipa ya damu na kuwa chanzo cha uharibifu mkubwa kwenye mfumo wa mzunguko wa damu. 

Muda wa kusubiri

Swali ni je, seli za beta hupumzika kwa muda gani kabla ya kuanza kufanya tena kazi? Muda wa haya mapumziko utatofautiana kati ya mtu na mtu kulingana na muda aliodumu na sukari yake kabla ya kuchukua hatua za kupumzisha hizo seli. Kwa bahati mbaya watu wengi huishi na mlundikano wa sukari kwenye damu kwa muda mrefu kabla ya kubainika kuwa ana tatizo hilo. Hii ni kutokana na ukweli kuwa baadhi ya dalili za kuwepo kwa sukari nyingi kwenye damu zinaweza pia zikasababishwa na magonjwa mengine. Kwa bahati mbaya ni madaktari wachache wanaokumbuka kuwapima wagonjwa wao kisukari pale wanakutana nao. Hii inaweza ikapelekea mtu kuishi na kisukari muda mrefu sana kabla ya hatimaye kugunduliwa kuwa anacho.

Chukua hatua

Jambo la msingi ni kwamba kama unataka kuzuia usipate tatizo la kisukari au unataka tatizo hilo liondoke mapema kadri iwezekanvyo baada ya kubainika, basi unalazimika kuchukua hatua stahiki. Hatua hizi ni pamoja na:

1. Kupunguza sana ulaji wa vyakula tulivyotaja hapo juu. Hatua hii itakusaidia kujikinga na tatizo la kisukari katika maisha yako yote.

2. Kama huwezi kupunguza vyakula tulivyovitaja hapo juu, basi jitahidi kupima sukari walau mara moja kila baada ya majuma mawili. Hatua hii itakusaidia kugundua mapema kuwa tayari umeshapata tatizo na itakusaidia kuchukua hatua mapema za kuacha kula vyakula ambavyo vinalisumu kongosho lako. Kadri unavyochukua hatua mapema ndivyo itakavyokuwa rahisi kwa seli za beta katika kongosho lako kurejea katika hali yake ya kawaida.

3. Kama wewe tayari ni mgonjwa wa kisukari cha ukubwani na unataka upone na kuachana na matumizi ya kila siku ya dawa (ambazo aghalabu huwa na athari mbaya za pembeni), basi achana na ulaji wa vyakula tulivyotaja hapo juu. Hatua hii itaanzisha mchakato wa kupumzisha seli za beta za kongosho lako na kama zilikuwa hazijaharibika kabisa, baada ya muda zitarejea katika kufanya kazi kama kawaida.

Sasa tule nini?

Wagonjwa wengi wenye kisukari huishi maisha magumu sana, pale wanapotaka kuchukua hatua kuondokana na kisukari chao kwa njia ya kubadilisha lishe, hususan wanapokuwa mbali na makaazi yao. Tatizo ni kwamba jamii haijui kabisa kuwa ugonjwa wa sukari hivi sasa ni tatizo kubwa na kwa hivyo migahawa mingi haijaweka kabisa mazingira ya kuweza kuwahudumia watu wenye kisukari. Hata hivyo kama unajua aina ya chakula unachopaswa kula unaweza ukachukua hatua ya kuzungumza na hao wenye migahawa na walio wengi wako tayari kukusaidia.

Kwa ujumla mtu anayetaka kuachana na kisukari alichonacho anapaswa kula aina ya lishe inayoitwa ketogenic. Hii ni lishe ambayo hujumuisha protini kidogo, kiasi kikubwa cha mchanganyiko wa mboga za majani, na kiasi cha kutosha cha mafuta koza.

Protini kidogo tu yatosha!

Ni muhimu kuzingatia kuwa mwili hauhitaji protini nyingi. Kiasi kingi cha protini kina madhara kiafya kutokana na chakula hiki kuzalisha kiasi kikubwa sana cha tindikali ndani ya mwili. Baadhi ya taifiti zimeonyesha kuwa kiasi cha gramu 27 tu za protini kwa siku zinatosha. Hawa wanadai kuwa kuasi cha protini kinapozidi hapo mzigo wa tindikali mwilini unakuwa ni mkubwa mno kiasi kwamba mifupa ya mwili inaanza kuachia madini ya kalisi (calcium) kuingia katika mzunguko wa damu ili kusaidia kuzimua hiyo tindikali. Hata hivyo kundi kubwa la watafiti hupendekeza kati ya gramu 50 na 70 tu kwa siku. Vyakula vya protini ni pamoja na nyama (aina zote), maziwa, mayai, samaki, na wadudu kama senene, nakadhalika. Kuna baadhi ya vyakula ambavyo asili yake ni mimea ambavyo vimebea pia kiasi kikubwa sana cha protini. Hivi ni vile vya jamii ya kunde mathalani soya, maharage, kunde zenyewe, njegere, nakadhalika.

Sasa nitembee na mzani?

Ukweli wa mambo ni kwamba huhitaji kutembea na mzani. Hakikisha tu kwamba kiasi cha 80% ya nafasi katika sahani yako ya chakula kimechukuliwa na mchanganyiko wa mboga za majani, ikiwezekana 50% - 75% ya hizo mboga ziwe katika hali ya ubichi (vegetable salad). Katika ile 20% ya nafasi iliyobaki nusu inaweza kuchukuliwa na chakula cha protini chochote na nusu inaweza kuchukuliwa na mafuta koza yoyote uliyonayo.

No comments:

Post a Comment