Friday, June 10, 2016

UNAWEZA KABISA KUEPUKANA NA KISUKARI CHA UKUBWANI



CHIMBUKO LA KISUKARI NI CHAKULA KISICHOFAA!

Chakula ambacho ni bora kabisa kwa mtu mmoja, kinaweza kuwa sumu baridi kwa mtu mwingine, na kumletea madhara endelevu katika maisha yake. Kwa muktadha huu basi hakuna chakula bora kwa kila mtu! Chakula ni bora kwa mtu kama baada ya kukitumia mwili utakipokea vizuri, ukafyonza virutubisho, na kikasaidia kuimarisha afya ya huyo mlaji.

Ni vigumu kujua aina ya chakula inayokufaa, bila kujua jinsi mwili wako unavyochakata chakula. Kimsingi watafiti wamebaini makundi makuu matatu ya watu kuhusiana na jinsi miili inavyochakata chakula. Kundi la kwanza ni la wachakataji wa protini. Hawa miili yao inakubaliana zaidi na vyakula vya protini. Kwa watu wa kundi hili vyakula vya wanga, na hususan vile vilivyochakatwa na kuchujwa kwa kiwango kikubwa (highly processed and refined), ni sumu baridi ambayo itawapelekea kuugua maradhi mengi ya kimfumo.

Kundi la pili ni la wachakataji wa wanga. Hawa miili yao inakubaliana zaidi na vyakula vya wanga. Kwa watu wa kundi hili vyakula vya protini, na hususan vile vilivyochakatwa na kuhifadhiwa kwa ajili ya kuwa na muda mrefu wa matumizi, ni sumu baridi ambayo itawapelekea kuugua maradhi mengi ya kimfumo. Kundi la tatu ni la wachakataji wa vyakula vya protini na wanga kwa viwango sawa. Kundi hili kidogo lina bahati kwa maana halidhuriwi kwa wepesi na vyakula vilivyoko katika yale makundi mawili ya mwanzo.

Moja ya magonjwa yanayosababishwa na mkanganyiko huu katika kula ni ugonjwa wa kisukari. Mchakataji wa protini anapokula chakula cha wanga, kasi ya kuchakata wanga huo ni kubwa mno ikilinganishwa na mlaji mwenzake ambaye ni mchakataji wa wanga. Kasi hiyo hupelekea kiwango cha sukari kinachoingia katika mzunguko wa damu ndani ya muda mfupi kuwa kikubwa sana. Kutokana na hali hii kongosho hulazimika kufanya kazi ya ziada kuzalisha kiwango kikubwa cha insulin (homoni ya kuondoa sukari kwenye damu na kuipeleka kwenye seli ili itumike kutengenezea nishati), ili kukabiliana na ongezeko hilo. 

Hali hii ikijirudia rudia mara kwa mara kongosho huchoka na kuanza kufanya kazi chini ya kiwango; au wakati mwingine vipokezi vya sukari katika seli (receptors) hushindwa kuendana na kasi ya kuletewa sukari kwa ajili ya matumizi ya seli, na huishia kuikataa sukari hiyo. Hali hii kitaalamu hujulikana kama insulin resistance, au pingamizi dhidi ya insulin kwa tafsri isiyo rasmi. Kuna baadhi ya nyakati yote mawili hutokea kwa wakati mmoja, yaani kongosho linafanya kazi chini ya kiwango, na pia mgonjwa anakabiliwa na pingamizi dhidi ya insulin.

Hivi karibuni imebainika kuwa moja ya sababu kubwa sana zinazopelekea vipokezi vya seli vikashindwa kupokea sukari inayoletwa ni kitu kinachoitwa mfuro (inflammation). Mfuro ni uvimbe kama lengelenge hivi. Mfano wa mfuro ni pale unapojikwaa au kujigonga usoni na mwili ukaumuka na kutengeneza nundu. Vichocheo vya kusababisha mfuro kwenye seli viko vingi lakini baadhi ya hivi ni vyakula tunavyokula kila siku. Vyakula hivi ni pamoja na sukari, wanga uiliochakatwa kwa kiwango kikubwa, na mafuta ya mbegu (alizeti, ufuta, karanga, pamba, mawese, nakadhalika) yanapotumiwa kwa ajili ya kupikia. Sababu nyingine ni maambukizi ya vimelea vya maradhi mbalimbali.

Wataalamu wameyagawanya magonjwa ya kisukari katika makundi makuu matatu. Makundi haya ni:
  1. Kisukari cha aina ya kwanza (type 1 diabetes). Hiki ni kisukari kinachojitokeza mapema (kwa kawaida kabla ya mtu kufika miaka 40), mara nyingi ikiwa ni katika kipindi cha utoto na ujana wa chini ya miaka 20. Katika aina hii ya kisukari mwili wa mhusika unaacha kuzalisha kabisa homoni ya insulin na hivyo kumlazimu mgonjwa kuishi kwa kudunga sindano za insulin kila siku.

  1. Kisukari cha aina ya pili (type 2 diabetes). Kiashiria kikubwa katika aina hii ya kisukari ni kwamba mwili hauzalishi insulin ya kutosheleza mahitaji, au vipokezi (receptors) vya sukari katika seli havifanyi kazi kwa kiwango kinachotakiwa. Zaidi ya asilimia 90 ya wagonjwa wote wa kisukari duniani wanaugua aina hii ya kisukari.

  1. Kisukari cha ujauzito (gestational diabetes). Hiki ni kisukari kinachowakumba baadhi wanawake pale wanapokuwa wajawazito. Wakati  wa ujazito baadhi ya wanawake huwa na kiwango kikubwa cha sukari kwenye mzunguko wa damu kuliko inavyotakiwa na wanaweza wakalazimika kutumia matibabu ili wasidhurike. Kutotambua kuweko kwa kisukari hiki na kukitibu kunaweza kusababisha matatizo wakati wa kujifungua. Moja ya madhara ya aina hii ya kisukari ni kuzaliwa watoto wenye miili mikubwa kuliko kawaida.

Kisukari ni ‘ugonjwa’ unaotisha. Ni ‘ugonjwa’ unaotisha kutokana na sifa zake. Sifa hizi ni pamoja na kutokuwa na dawa ya uhakika, kumlazimisha mgonjwa abadilishe mwenendo wake wa maisha kwa kiasi kikubwa, kusababisha mlolongo wa madhara mengine kibao ya kiafya ndani ya mwli, kuongeza gharama za maisha kwa mgonjwa, na ile hali ya kugeuka kuwa janga la kijamii.

Tunasema kisukari hakina dawa ya uhakika kwa kuwa ulimwengu wa tiba za kisasa umeshindwa kuja na dawa za aina hiyo hadi sasa. Dawa zilizoko ni zile za kumsaidia mgonjwa kushusha sukari iliyolundikana kwenye damu yake, ili iende katika viwango vinavyokubalika. Hata hivyo historia inaonyesha kuwa baadhi ya dawa hizi siyo salama, na hatima yake zinamsababishia mtumiaji madhara mengine ya kiafya ikiwa ni pamoja na kumwongezea uwezekano wa kupoteza maisha.

Avandia (rosiglitazone) ni moja ya dawa hizo. Mauzo ya dawa hii ambayo enzi zake ilikuwa ni moja ya dawa maarufu sana za kifamasia kwa ajili ua ugonjwa wa kisukari, yalifikia kiasi cha dola za Kimarekani bilioni 3.2 mnamo mwaka 2006. Baada ya hapo ziliibuka taarifa za kitafiti kwamba dawa hii ilikuwa inasababisha madhara makubwa ya kiafya kwa mtumiaji kama vile ongezeko la hatari ya shambulizi la moyo (heart attack), wepesi wa kuvunjika mifupa na hususan ile ya mikononi juu ya kiwiko, uharibifu wa macho, kiharusi na uharibifu wa ini kutokana na ongezeko la sumu. Inakadiriwa kuwa ndani ya Marekani peke yake kati ya mwaka 1999 na mwaka 2006 dawa hii ilisababisha mashambulizi ya moyo (heart attacks) na vifo kati ya 60,000 na 200,000.

Japokuwa baadhi ya matatibu wa dawa za asili na zile za tiba mbadala wanadai kuwa wanatibu ugonjwa huu, madai haya yanapaswa kuchukuliwa kwa tahadhari. Ni kweli kuwa mtu anaweza kuwa na dawa ya kuondoa sababu moja au zaidi ya kisukari na hivyo kumsaidia mtumiaji kuondokana na dalili zote za ugonjwa huo. Hata hivyo hii haina maana kwamba dawa hiyo itamtibu kila mgonjwa wa kisukari. Kwa kifupi ni kwamba kundi la wenye kisukari kilichosababishwa na sababu zinazoguswa na dawa husika watapona, na wengine wenye kisukari kilichosababishwa na sababu zisozoguswa na dawa hiyo hawatapona.

Mazoea yana tabu sana. Tulio wengi hatuli chakula kwa kuzingatia kanuni za afya bali tunakula kwa ajili ya mazoea na kulenga ladha. Mgonjwa wa kisukari mwenye nia ya kuidhibiti hali hiyo analazimika kuachana kabisa na kula kwa mazoea na kulenga ladha. Anatakiwa ajue kuwa vyakula vyote vya wanga, na hususan vile vilivyochakatwa kwa kiwango kikubwa, vina madhara makubwa kwake na anatakiwa kuviendea kwa tahadhari kubwa. Hali hii huwa ni chanzo kikubwa cha kufadhaika kwa baadhi ya watu ambao wamepata ugonjwa wa kisukari. Baadhi yao huuliza kwa ghadhabu : ‘sasa utakula nini???!’ na kuendelea kula vyakula vyao walivyozoea huku wakisaidiwa kisaikolojia na kimwili na vidonge wanavyopewa hospitalini na madaktari wao. Waathirika wengi wa madawa kama avandia ni wale wanaoangukia katika kundi hili.

Kisukari pia kinatisha kwa kuwa kinasababisha mololongo wa matatizo mengine kibao ya kiafya. Matatizo haya ni pamoja na uharibifu wa macho unaotambulishwa na magonjwa kama glaucoma (uharibifu wa neva za jicho), cataracts (ukungu kwenye lenzi ya jicho),  retinopathy (uharibifu mkubwa katika retina ya jicho), nakadhalika.  Matatizo ya miguu yanayotambulishwa na magonjwa kama neurapathy(maumivu yatokanayo na uharibifu wa mishipa ya fahamu), ulcers (vidonda sugu), gangrene (mkusanyiko wa tishu zilizokufa kutokana na kutofikiwa na mzunguko wa damu), nakadhalika. Matatizo mengine ni yale ya magonjwa ya ngozi na magonjwa ya moyo.

Faraja ya ugonjwa wa sukari ni kuufatilia kwa makini. Hii ina maana kuwa ni muhimu kufanya kipimo kila siku, ikiwezekana hata mara mbili au tatu kwa siku. Kutokana na hali hii gharama za kuufuatilia ugonjwa huu ni kubwa na huathiri kwa kiasi kikubwa hali ya kiuchumi ya mgonjwa. Kwa mfano tu, hivi sasa katika zahanati na vituo vingi vya afya, gharama za kupima kisukari kwa mara moja ni kati ya shilingi 2,000.00 na shilingi 2,500.00. Unapomwambia mtu apime mara tatu kwa siku maana yake atumie kati ya shilingi 6,000 na shilingi 7,500.00 kila siku!

Mwisho kisukari kinatisha kwa sababu taratibu kinaonekana kunyemelea hadhi ya kuwa ni janga kubwa sana la kijamii. Katika pande zote za dunia kisukari kinaongezeka badala ya kupungua. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani, dunia inatarajiwa kuwa na wagonjwa wa kisukari 366,000,000 mwaka 2030 kutoka wagonjwa 171,000,000 waliokuwepo mwaka 2,000. Hili ni  ongezeko la aslimia 53! Tanzania, ambayo mwaka 2,000 ilikuwa na wagonjwa 201,600 inatarajiwa kuwa na wagonjwa 605,000 mwaka 2030, ikiwa ni ongezeko la 66.7%

Hata hivyo janga la kisukari linaoonekana kuzikumba zaidi zile nchi ambazo raia wao wanapendelea mno vyakula vya wanga katika mitindo tofauti- soda, pasta, doughnut, keki, mikate, lambalamba, nakadhalika. Nchi kama Italy uwiano kati ya Wataliano wanaoumwa kisukari na wale ambao hawaumwi ni 1:14!. Inawezekana sababu kubwa ikawa ni piza, pasta na spaghetti. Hivi ni vyakula vinavyotengenezwa kwa ngano na Wataliano wanavifakamia kwa wingi.

Marekani uwiano wao ni 1:17. Hii nayo ni jamii ambayo imelogewa soda, doughnut, chips, pizza, na vyakula vingine vya wanga vilivyochakatwa kwa kiwango cha juu. India uwiano wao ni 1:39. Hawa nao ni mabingwa wa vitu vitamu. Wahindi ni wafakamiaji wa tamutamu za kila aina na sifa kuu ya tamutamu hizi ni wingi wa sukari, ngano, mafuta na rangi.

Tanzania ina uwiano wa 1:238. Huu ni uwiano mzuri sana ukilinganisha na nchi tulizotangulia kuzitaja. Sababu ya uwiano huu mzuri ni nini wakati kimsingi sehemu kubwa ya Watanzania ni wala wanga zaidi kutokana na hali zao za kiuchumi? Nadhani sababu kubwa ni ukweli kwamba Watanzania wengi ni wakaazi wa vijijini na kimsingi pamoja na kwamba sehemu kuwa ya chakula chao ni wanga, lakini kutokana na sababu za kiuchumi, wanalazimika kuula wanga huo katika mfumo ambao haujachakatwa.

Kuepukana na ugonjwa wa kisukari ni muhimu kufanya kipimo cha kutambua aina ya mwili wako katika kuchakata vyakula (metabolic typing test) na iwapo utagundulika kuwa wewe ni mchakataji wa protini haraka uchukue hatua za kupunguza kwa kiwango kikubwa ulaji wa wanga, na hasa ule ambao umechakatwa kwa kiwango kikubwa. Nafasi ya wanga (kwa ajili ya kuzalisha nishati ya matumizi ya mwili) ichukuliwe na mafuta bora ya kula – nazi, siagi, samli, zaituni. Nafasi ya wanga kwa ajili ya kujaza tumbo ichukuliwe na mboga mchanganyiko za majani, na pale ambapo uwezekano upo, sehemu kubwa ya mboga hizo iwe mbichi (salad). Mafuta ya kawaida (yale tuliyoyazoea) tunaweza kuendelea kuyatumia (siyo kwa kupikia) bali kwa kupambia saladi (salad dressing). 

Aidha kama wewe tayari ni mgonjwa wa kisukari, utanufaika sana kwa kuondoa wanga uliochakatwa katika orodha ya vyakula vyako na ukaingiza wanga ambao haujachakatwa, tena kwa kiwango kidogo sana kma mbadala wake. Kwa ajili ya kuupatia mwili nishati punguzo hilo la wanga lichukuliwe na ongezeko la mafuta bora ya kula – nazi, siagi, samli, na zaituni. Aidha nafasi ya kushiba ichukuliwe na wingi wa mchanganyiko wa mboga za majani, ikiwezekana sehemu kubwa ya mboga hizi iwe mbichi (salad).

Kama ilivyo kwa yule anayelenga kukwepa kuugua kisukari, mafuta ya kawaida (yale tuliyoyazoea) tunaweza kuendelea kuyatumia (siyo kwa kupikia) bali kwa kupambia saladi. Ushauri huu kuhusu mafuta ni kinyume kabisa na ushauri mnaopatiwa na madaktari wenu kuhusu mafuta ya kula. Hata hivyo kisayansi ndio ushauri sahihi. Mungu akipenda post yetu ijayo itazungumzia jambo hili kwa kina ili kuliweka katika mazingira ya kueleweka zaidi..

No comments:

Post a Comment